Kuandaa chakula cha kuku wa kienyeji kwa mbinu za kilimo-ikolojia

Kilimo

Ujumbe kwa mtangazaji

Taarifa kwa Mtangazaji

Mlo uliotengenezwa nyumbani wenye lishe kamili unaopatiwa kuku wa kienyeji huboresha ubora na ladha ya kuku wa kienyeji, huwafanya wapendwe na wateja, na huunda nafasi thabiti ya soko kwa wale wanaofuga kuku. Hii inasaidia kufanya kuku wa kienyeji kuwa maarufu zaidi katika masoko ya Tanzania kuliko kuku wa kisasa.

Soko kwa ajili ya kuku na mayai ya kienyeji nchini Tanzania ni bora zaidi kuliko soko la kuku wa kisasa, kwani walaji wanapendelea kuku wanaokula chakula cha asili au kienyeji, kuliko wale wanaolishwa mchanganyiko wa vyakula vya viwandani vilivyochanganywa na madawa.

Mwongozo huu utakusaidia kuelewa jinsi wafugaji wa kuku wa kienyeji kutoka Mkoa wa Dodoma wanavyoandaa chakula cha kuku wa kienyeji. Kuwalisha kuku wao kwa vyakula vinavyopatikana kwenye maeneo yao, kunawasaidia wafugaji kupambana na umasikini na kujipatia kipato kwenye kaya.

Mwongozo huu unatokana na mahojiano halisi. Unaweza kuutumia  kuandaa maelezo kwenye mada kama hiyo katika mkoa wako. Unaweza pia kutumia waigizaji wa sauti kuwasilisha muongozo huu kwenye kituo chako cha redio. Ukifanya hivyo, tafadhali waambie wasikilizaji wako mwanzoni mwa kipindi cha redio kuwa hizi ni sauti za waigizaji na sio sauti za wahojiwa halisi.

Kama ungependa kuunda vipindi kuhusu ufugaji wa kuku wa kienyeji, unaweza kuwahoji wafugaji wadogo wadogo na wataalamu wa ufugaji wa kuku katika eneo lako. Unaweza kufikiria kuwauliza maswali yafuatayo: 

  • Njia bora ya kulisha kuku wa kienyeji ni ipi? Je, lishe inapaswa kuwa tofauti kwa kuku wadogo na wakubwa?
  • Wakulima wanapaswa kuwalinda vipi kuku wa kienyeji dhidi ya magonjwa?
  • Wakulima wanawezaje kujenga mabanda yanayofaa ili kufuga kuku wa kienyeji kwa usalama na kuwafanya wawe na afya?

Script

MTANGAZAJI:
Habari msikilizaji, na karibu kwenye kipindi cha leo. Ingawa muundo wa kijenetiki wa kuku wa kienyeji ni moja ya sababu zinazoathiri ubora wa nyama na mayai yao, sababu nyingine muhimu ni aina ya chakula wanachokula. Hii ni miongoni mwa mambo yanayowatofautisha kuku wa kienyeji na aina nyingine za kuku, ikiwemo kuku wa kisasa.

Iwe nyama ya kuku wa kienyeji inatumika kupikwa kwenye mchuzi, kuchomwa au kuokwa, haihitaji vihifadhi au viungo vingi ili iwe na ladha nzuri. Inapendwa sana kiasi kwamba wakati mwingine watu husafiri umbali mrefu kupata nyama au mayai wanayoyapenda. Hili ni kweli hasa kwa watu wengi wanaoishi katika maeneo ambapo kuku wa kisasa ndio wanapatikana kwa wingi. Watu wengi wanafahamu kuwa kuku wa kienyeji hula vyakula vinavyopatikana katika mazingira ya asili yanayowazunguka, na kwamba hali hii husababisha upatikanaji wa nyama na mayai yenye ubora wa hali ya juu. Leo, tutaangalia jinsi wakulima wanavyoweza kuandaa chakula cha kuku wa kienyeji.

Katika kipindi hiki, tutafanya mahojiano na watu watano. Anna Msenduki ni mtaalamu kutoka ofisi ya kilimo ya Wilaya ya Mpwapwa, Mkoa wa Dodoma. Pia tuna wakulima watatu kutoka kijiji cha Hogoro katika Wilaya ya Kongwa: Petro, Silvester Gidion, na Juktani Simon. Aidha, tutazungumza na Veronika Masaka, mkulima kutoka Mkoa wa Dodoma, katikati mwa Tanzania. Mabibi na mabwana, mnakaribishwa sana.

Veronica Masaka ni mfugaji wa kuku wa kienyeji ambaye atazungumzia jinsi anavyowalisha kuku wake wa kienyeji.

 

VERONIKA MASAKA:
Nimekuwa mfugaji wa kuku aliyefanikiwa kwa kipindi cha miaka kumi sasa kama sehemu ya shughuli zangu za kilimo biashara.

MTANGAZAJI:
Unawalisha nini kuku wako wa kienyeji?

VERONIKA MASAKA:
Kuku wangu hutumia takriban masaa 10 nje ya banda, na wakati wote huu wanajitafutia chakula.

Kila mara ninahakikisha kuna maji ya kutosha nje ya banda. Kwa njia hii, wanapohitaji maji, wanaweza kuyapata kwa urahisi badala ya kukaa muda mrefu pasipo kunywa maji au kunywa maji machafu na/au yaliyochafuliwa ambayo yanaweza kusababisha magonjwa.

Wanapotoka kwenye banda saa kumi na mbili asubuhi Jumatatu, nawapa chakula kidogo cha mabaki ya chakula kwenye bakuli lao la chakula.

Baada ya hapo, nawaruhusu waende kutafuta vyanzo vingine vya lishe wenyewe nnje kwa sababu kuna vyanzo vingi vya wao kupata chakula katika eneo la karibu hadi wanaporudi kwenye banda lao jioni.

MTANGAZAJI:
Unawapa chakula gani kingine kuku wako wa kienyeji?

VERONIKA MASAKA:
Natafuta majani ya mboga na mboga mbichi kama spinach na kabichi, lakini pia mara kwa mara nakusanya majani mengine, kwa mfano, majani ya majani ya magugu, kisha nayachanganya au kuyaweka katika eneo ambalo kuku wanapopumzika ili kupunguza gharama ya chakula. Kuku hupata vitamini na madini ya ziada kama kalsiamu kutoka kwa majani ya mboga mboga na kutoka kwenye eneo la karibu na nyumba.

MTANGAZAJI:
Unawapa chakula gani kingine isipokuwa mabaki ya chakula na majani ya mboga mboga?

VERONIKA MASAKA:
Nawapa matunda na mabaki ya matunda ambayo nakusanya kutoka kwa majirani asubuhi. Ninayapeleka kwa kuku wangu asubuhi kabla hawajaondoka kutafuta vyakula vingine.

Matunda hutoa virutubisho mbalimbali kama vile vitamini C vinavyowalinda dhidi ya magonjwa.

Yanaweza kuwa mapera, ndizi, au matunda mengine tofauti. Kuku wanapenda matunda kila mara na huwa wanayala na kumaliza kabisa.

MTANGAZAJI:
Unawapa chakula gani kuku wanapokuwa nje?

VERONIKA MASAKA:
Wanapokuwa nje, kuku hujipatia chakula wenyewe—kama vile mdudu wadogo, majani, na mbegu za miti ya matunda.

MTANGAZAJI:
Unatumia kiasi gani kununua chakula kwa ajili ya kuku wako?

VERONIKA MASAKA:
Sinunui chakula chochote kwa sababu ninatumia mabaki ya chakula na kuku huenda nnje kujitafutia chakula chao wenyewe. Nimekuwa nikiuza nyama ya kuku wa kienyeji sokoni kwa sababu ni tamu, na pia nimekuwa nikitumia kuku wa kienyeji kama chanzo cha chakula nyumbani. Kwa hivyo, nimefaidika sana.

MTANGAZAJI:
Unafanya nini ikiwa huna mabaki ya chakula ya kuwapa asubuhi kabla ya kuwaruhusu kwenda nnje?

 

 

VERONIKA MASAKA:
Wakati ambapo sina mabaki ya chakula, ninawatoa nnje mapema asubuhi na kuwaruhusu wajitafutie chakula chao wenyewe.

MTANGAZAJI:
Mpendwa msikilizaji, leo katika kipindi chetu tunajifunza kuhusu lishe kwa ajili ya kuku wa kienyeji. Sasa tuko na Silvester Gidion, mfugaji kutoka Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma, Tanzania. Atatuambia ni aina gani ya chakula anachowapa kuku wake wa kienyeji.

SILVESTER GIDION:
Asante sana. Katika kijiji chetu, tunawapa kuku wa kienyeji mahindi na mtama au mabaki ya jikoni.

MTANGAZAJI:
Unawalisha vipi chakula kuku wa kienyeji ikiwa unawafungia ndani ya nyumba?

SILVESTER GIDION:
Mwanzo, nilianza na kuku sitini, na niliandaa kilo tano za unga wa mahindi mchanganyiko na virutubisho vingine. Baadaye, niliongeza kilo tano za mtama na lita tatu au nne za maji kwa ajili ya kunywa. Hichi ndiyo kiasi cha chakula ambacho kuku sitini hula kwa siku moja.

MTANGAZAJI:
Je, ratiba yako ya kila siku ya kuwahudumia kuku wa kienyeji iko vipi?

SILVESTER GIDION:
Tunaamka asubuhi saa 12:00 na kusafisha makazi yao na kuandaa mahindi kwa ajili yao hadi saa sita mchana. Saa 10:00 asubuhi, tunaweka maji kwenye chombo chao kwa sababu kuku wetu wa kienyeji hawatoki kwa kipindi hichi.

Chakula tunachowapa kina virutubisho ambavyo wanavikosa kutoka kwenye chakula ambacho wanajitafutia wenyewe na kinajumuisha mtama na mahindi.

Jioni, tunawaandalia maji ya kunywa na kusafisha makazi yao kwa mara ya pili ili kuhakikisha wanalala mahali safi na salama.

Tunafanya hivi hasa ili kulinda kuku wadogo kutokupata magonjwa kutokana na makazi machafu, na pia kuwalinda wasile uchafu ambao pia unaweza kusababisha magonjwa.

Daima tunawatenga kuku wakubwa na wadogo ili tuweze kuwapa chakula tofauti. Mara nyingi, tunawapa chakula tofauti kuku wadogo na wakubwa, hasa wale walioko kwenye mabanda tuliyojenga.

MTANGAZAJI:
Ni faida gani umezipata kutokana na kufuga kuku wa kienyeji?

SILVESTER GIDION:
Niliweza kujenga nyumba ya familia kupitia kuuza kuku na mayai.

MTANGAZAJI:
Sasa tutazungumza na Juktani Miagi, ambaye pia anafuga kuku wa kienyeji. Atatuambia jinsi anawahudumia kuku wa kienyeji pale wanapopata magonjwa.

JUKTAN MIAGI:
Kwanza, hatukupokea ushauri wowote kutoka kwa maafisa wa ugani juu ya jinsi ya kutibu kuku wa kienyeji. Tulitumia dawa za kienyeji za mimea ambazo tulichanganya na maji na kuziweka kwenye maji ya kunywa ya kuku. Au tulitumia majani ya mihogo. Lakini pale magonjwa yalipozidi kuwa ni changamoto, tulianza kutafuta wataalamu kwa ajili ya matibabu zaidi.

MTANGAZAJI:
Ni hatua gani katika kutibu ugonjwa unapoita mtaalamu?

JUKTAN MIEGI:
Ikiwa tunashindwa kutibu ugonjwa, tunawaita maafisa kutoa matibabu zaidi au chanjo kwa kuku wenye afya.

MTANGAZAJI:
Nini hutokea baada ya afisa kuja na kutibu au kutoa chanjo kwa kuku wako?

JUKTAN MIAGI:
Kuku wanapopatiwa matibabu kwa usahihi au kupatiwa chanjo, ugonjwa hupotea na kuku wanaishi vizuri bila matatizo yoyote. Maafisa wa mifugo hutufundisha kwamba tunapaswa kutoa chanjo kwa kuku wetu mara kwa mara kabla ya ugonjwa kuwapata.

MTANGAZAJI:
Kuku anapaswa kupatiwa chanjo akiwa na umri gani? Je, afisa mifugo aliwapa aina maalum ya chanjo?

JUKTAN MIAGI:
Walipatiwa chanjo za ugonjwa wa Kideri, Gumboroa, na mafua, kwa sababu haya ni magonjwa yanayojirudia mara kwa mara na kusababisha shida kubwa kwa kuku. Tulifundishwa kuwachanja kuku wanapokuwa na umri wa siku 3–7. Kuku wanakuwa hatarini zaidi kupata magonjwa wakiwa katika umri huu, na miezi ya baridi katika eneo letu ndio wakati wanapopata shida kubwa zaidi.

MTANGAZAJI:
Jesca Peter pia anafuga kuku wa kienyeji. Anaeleza jinsi yeye na mumewe wanavyotengeneza chakula cha kuku wa kienyeji na jinsi kuku hao wanavyopatwa na magonjwa.

JESCA PETRO:
Kila siku asubuhi, tunawalisha kuku kwa mahindi yaliyosagwa kwenye machine ya kusaga, na pia tunawalisha mtama. Tunawaalisha mara mbili kwa siku, asubuhi na jioni.

MTANGAZAJI:
Kwa nini mnatumia mahindi na mtama? Je, kuku wanakula vizuri chakula hiki, au kuna matatizo yoyote?

JESCA PETRO:
Vifaranga hawawezi kula nafaka yote, lakini kwa kuku wakubwa, hakuna tatizo lolote kabisa.

MTANGAZAJI:
Mnafanya kazi vipi na maafisa wa mifugo na kilimo?

SILVESTER GIDION:
Maafisa ugani hututembelea kwa ratiba, au tunapohitaji msaada baada ya kugundua tatizo. Tunawapigia simu za mkononi, na wao huja kuchunguza matatizo na kutoa maoni juu ya namna bora ya kuzuia mambo yasizidi kuwa mabaya.

MTANGAZAJI:
Wakulima wanapaswa kujenga vipi mabanda ya kuku wa kienyeji ili waweze kula vizuri, kukuwa na kuwa na Afya?

SILVESTER GIDION:
Kuna aina mbili za mabanda ya kuku: mabanda huru na mabanda ya vyumba. Mabanda huru ni ya urefu wa mita 15 na upana wa mita tano, makubwa vya kutosha ili kuku 100 waishi vizuri. Tunatumia nyavu za kuku, matofali, bati, na mbao kujenga banda huru.

Mabanda ya vyumba yana urefu kuanzia nusu mita hadi mita moja na nusu na upana wa mita tano, na yana vyumba viwili. Vinakuwa na vifaa maalum vya kulisha ambavyo huzuia chakula kumwagika, pamoja na vifaa vya kutoa maji.

Tunafanya usafi wa mabanda kila asubuhi.

MTANGAZAJI:
Je, unawalinda vipi kuku wa kienyeji dhidi ya magonjwa?

SILVESTER GIDION:
Tunatumia chanjo, na tunawatenga kuku wagonjwa kutoka kwenye kundi ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa.

Pia, tunatenga kuku wadogo kutoka sehemu ambapo kuku wakubwa wanakaa.

MTANGAZAJI:
Unawapa chakula gani kuku wadogo?

SILVESTER GIDION:
Kwa kuku wadogo, tunakoboa mahindi kisha kuyachuja ili kupata chakula kidogo ambacho kuku wadogo wanaweza kumeza.

MTANGAZAJI:
Sasa tutazungumza na Afisa Mifugo kutoka Wilaya ya Mpwapwa katika Mkoa wa Dodoma, ambaye atatueleza kuhusu chakula kinachopendekezwa kwa ajili kuku wa asili.

ANNA ANTHONY MSENDUKI:
Jina langu ni Anna Anthony, na mimi ni daktari wa mifugo ninayehusika na kutoa elimu na ushauri kuhusu ufugaji wa kuku wa asili au kuku wa kienyeji pamoja na wanyama wengine.

Lishe ya kuku wa kienyeji au wa asili haitofautiani sana na ile ya kuku wa kisasa (chotara). Kwa kawaida, kuku wa asili hufugwa kwa mfumo wa kuachiwa huru, wakati kuku wa chotara hufugwa kwa mfumo wa nusu kufungiwa na nusu kuachiwa, na mara nyingi hufugwa pamoja na kuku wa asili.

Kwa upande wa chakula, aina hizi mbili za kuku hazina tofauti kubwa. Lengo ni kuwafuga kibiashara, hivyo tunataka wakue haraka na wapate virutubisho sahihi. Kwa mfano, chakula cha kuku kinaweza kujumuisha mtama, uwele, chokaa, madini yaliyochanganywa tayari, mashudu ya mbegu, na chumvi. Hii husaidia kuku kupata virutubisho na madini muhimu kwa ajili ya kujenga miili yao.

Aidha, kwa kuwa kuku hufugwa kwa mfumo wa nusu kufungiwa na nusu kuachiwa, hupata pia wadudu wa aina mbalimbali, ambao huongeza virutubisho muhimu katika mlo wao.

MTANGAZAJI:
Kuku wa kienyeji wanapaswa kula kiasi gani cha chakula kwa siku?

MTANGAZAJI:
Je, vipi kuhusu kuku wengine wadogo?

ANNA ANTHONY MSENDUKI:
Hapa ni mchanganyiko wa chakula kwa kuku wa kienyeji wenye umri wa miezi mitatu au minne. Pia kuna viambato saba katika mchanganyiko huu.

Kwanza, ongeza kilo 25 za pumba za mahindi au mtama; pili, ongeza kilo 44 za mtama au mahindi; tatu, ongeza kilo 17 za mashudu ya mbegu za alizeti, mashudu ya ufuta, mashudu ya pamba, au mashudu ya karanga; nne, ongeza kilo 3.25 za unga wa mifupa au chokaa; tano, ongeza kilo 10 za dagaa au unga wa samaki; sita, ongeza robo kilo ya chumvi ya jikoni; na mwisho, ongeza nusu kilo ya virutubisho. Mchanganyiko huu pia unatoa kilo 100 za chakula.

MTANGAZAJI:
Je, vipi kuhusu kuku wa kienyeji wenye umri wa miezi mitano hadi sita?

ANNA ANTHONY MSENDUKI:
Kwa kuku wa kienyeji wenye umri wa miezi mitano hadi sita, unawapatia mchanganyiko ufuatao hadi wauzwe. Una viambato sita:

Kwanza, unaongeza kilo 31 za pumba za mahindi au mtama; pili, ongeza kilo 38 za mashudu ya mbegu za alizeti, mashudu ya ufuta, mashudu ya pamba, au mashudu ya karanga; tatu, ongeza kilo 2.25 za unga wa mifupa au chokaa; nne, ongeza kilo 13 za dagaa au unga wa samaki; tano, ongeza nusu kilo ya chumvi ya jikoni; na sita, ongeza robo kilo ya virutubisho. Hii inatoa jumla ya kilo 100.

Ni muhimu kutambua kwamba mchanganyiko huu wa mwisho ni kwa ajili ya kuku wa kienyeji wanaofugwa kibiashara tu, na hufanya kuku kuwa na mafuta.

Lakini ikiwa unataka kuku wako wa kienyeji wakue haraka kwa mchanganyiko huu, anza kuwapa mwishoni mwa mwezi wa tatu. Baada ya hapo, unapaswa kuwapatia mchanganyiko ufuatao wenye viambato 10 ili kujiandaa kutaga mayai:

Kwanza, kilo 2 za dagaa; pili, kilo 2 za unga wa damu; tatu, kilo 8 za mashudu ya mbegu za ufuta; nne, kilo 5 za pumba za mahindi; tano, kilo 24 za mahindi; sita, kilo 5 za chokaa; saba, kilo 4 za unga wa mifupa; nane, gramu 150 za virutubisho kwa kuku wa mayai; tisa, gramu 50 za methionini; na mwisho, gramu 30 za chumvi.

MTANGAZAJI:
Ni kuku wapi ambao ni bora kuuza sasa hivi—kuku wa kisasa au kuku wa kienyeji?

ANNA ANTHONY MSENDUKI:
Kuku wa kienyeji ndio bora zaidi. Soko la kuku wa kienyeji lina mauzo makubwa zaidi kutokana na ubora wa nyama na mayai yake.

MTANGAZAJI:
Tumeifika mwishoni mwa kipindi chetu. Asanteni sana kwa kusikiliza kipandi hiki, na natumai mmejifunza mengi kuhusu jinsi ya kulisha na kufuga kuku wa kienyeji.

Katika kipindi hiki, tumeona kwamba wafugaji wanaweza kutumia mabaki ya chakula kuwapatia kuku wa kienyeji kabla ya kuwaachia kutoka kwenye mabanda yao ili wajitafutie chakula chao wenyewe.

Pia, tumeona kwamba kuku wa kienyeji wanaweza kulishwa mabaki ya matunda au matunda yenyewe.

Zaidi ya hayo, kuku wa kienyeji wanaweza kutumia muda mwingi nje ya mabanda, na wanaweza pia kupewa chakula wakiwa ndani ya banda, ikiwemo majani.

Mwishowe, wafugaji wanaofuga kuku wa kienyeji wanapaswa kuwa na mawasiliano ya karibu na maafisa mifugo ili kuwatarifu pale kuku wao watakapokuwa na matatizo ya magonjwa au kupata ushauri wa kitaalamu.

Acknowledgements

Imeandaliwa na: Method Charles, Mwandishi wa masuala ya Kilimo, Arusha, Tanzania

Imehaririwa na: Eliud M. A. Letungaa. Afisa Kilimo na Mifugo, Mtandao wa Vikundi vya Wakulima na wafugaji Mkoa wa Arusha (MVIWAARUSHA).

 

Vyanzo vya taarifa

Anna Msenduki, Afisa kilimo, Wilaya ya Mpwapwa, Mkoa wa Dodoma, Alihojiwa July 6, 2022.

Jesca Petro, Mkulima, Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma Region, Alihojiwa July 5, 2022.

Silvester Gidion, Mkulima, Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma, Alihojiwa July 5, 2022.

Juktani Miagi, Mkulima, Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma, Alihojiwa, July 5, 2022.

Veronika Masaka, farmer, Mvumi, Dodoma Region, interviewed Aug. 9, 2022.

 

Chanzo hichi kimeandaliwa  kwa msaada wa kifedha wa Taasisi ya Biovision.