Habari za kughushi: Jinsi ya kuzitambua na nini cha kufanya juu yake

Script

Save and edit this resource as a Word document

Habari za kughushi ni nini?

Watu wengi wanapenda kushiriki na marafiki hadithi, picha, video, na habari za simulizi kwenye mitandao ya kijamii. Unaweza kuwashirikisha watu kitu kwasababu unaona ni kitu cha kuchekesha au kwasababu unafikiri ni simulizi ya habari muhimu ambayo watu wengi zaidi katika mzunguko wako wa kijamii wanapaswa kujua.

Wakati mwingine watu wanashirikisha habari ambazo wanajua sio za kweli. Aina hii ya habari zisizo za kweli* inaweza kuenea kwa njia nyingi, kwa njia ya mtandao na nnje ya mtandao, kupitia njia mpya za mawasiliano na njia za zamani za mawasiliano. Televisheni, machapisho, redio, tovuti za habari mtandaoni – njia zote za mawasiliano zinaweza kueneza habari za kughushi.

Kama mtangazaji, kabla ya kushirikisha habari au picha au video, je! Unaacha kwanza na kuchambua maelezo? Unauliza yaliyomo na unajiuliza ikiwa ni sahihi kabisa? Sio kila kitu tunachokiona au kusoma ni kweli.

Hadithi za uwongo zinaweza kusambaa haraka sana na ni shida kubwa. Hii imekuwa ukweli wa bahati mbaya ya maisha ya kila siku kwenye mtandao na nnje ya mtandao kote ulimwenguni, kwani watu, makampuni, na vyombo vya habari hutunga hadithi ambazo sio za kweli kwa faida ya kisiasa au ya kibinafsi, au kwasababu zingine tofauti. Hali hii inaitwa “habari ya kughushi,” na kama mtangazaji, ni muhimu sana ujue jinsi ya kuigundua, wakati haujachangia wewe mwenyewe kwenye habari hiyo.

Kufanya mambo kuwa magumu zaidi, neno “habari za kughushi” pia wakati mwingine hutumika kutoa shaka juu ya habari halali kutoka kwa maoni ya kisiasa yanayopingana.

Gazeti la New York Times linafafanua “habari za kughushi” kama habari zilizotengenezwa kwa kusudi la kudanganya, mara nyingi zinalenga kupata mvuto. Ni muhimu kutambua kuwa habari za kughushi SIO kitu sawa na habari zisizo sahihi, habari za ukweli zisizo sahihi. Hakuna mtangazaji au mwandishi wa habari ambaye ni mkamilifu na tunaweza sote kufanya makosa katika utafiti na kuripoti. Kwa kulinganisha, habari za kughushi ni habari zisizo za kweli ambazo zinasambazwa kwa makusudi.

Kuelewa habari za kughushi kunawezaje kunisaidia kuwatumikia vizuri wasikilizaji wangu?

  • Habari ni chombo muhimu sana cha kupeleka taarifa sahihi juu ya maswala ya kisiasa, kijamii na kisayansi. Habari zinapotolewa kwa usahihi na kwa usawa, huwapa wasikilizaji fursa ya kuchukua taarifa na kuunda maoni yao wenyewe na hoja juu ya hali au tukio.
  • Kwa kutangaza habari sahihi tu, zilizofanyiwa utafiti vizuri, unaweza kupata kuaminiwa na umma pamoja na wasikilizaji wako.

Ni kwa namna gani kuwa makini na habari za kughushi kunanisaidia kuzalisha vipindi bora?

  • Kama mtangazaji, ni muhimu sana kuwa unaelewa jinsi ya kugundua habari za kughushi ili kuepuka kuzisambaza kupitia vipindi vyako wewe mwenyewe. Kwa kuchagua taarifa za ukweli na sahihi kutoka kwenye taarifa ambazo unajua ni za uwongo au taarifa ambazo ni za mashaka na ambazo huwezi kuthibitisha kama ni za kweli na kwa kukusanya taarifa sahihi, unahakikisha kwamba vipindi vyako ni sahihi, madhubuti, vinavyofaa na vya kuaminika.

Ninaanzaje? (Jifunze zaidi kuhusu hoja hizi na zingine katika sehemu ya Maelezo hapa chini)

  1. Jinsi ya kutambua habari za kughushi
  2. Usiwe sehemu ya tatizo
  3. Umuhimu wa ukweli

Maelezo

1. Jinsi ya kutambua habari za kughushi

Pamoja na idadi kubwa ya habari za uwongo na habari za kughushi kuwa zinasambazwa ulimwenguni kote, ni kazi yako kama mtangazaji anayeheshimiwa kuchuja “habari za kughushi” kutoka kwenye “habari” na kuwasilisha ukweli kwa watazamaji wako kwa njia sahihi na inayohusika.

Hii ni namna ya kuuliza maswali kuhusu hadithi ambazo umewasilishiwa:

Kuwa na akili ya kukosoa

Mojawapo ya sababu kuu ambayo inachochea kusambaa kwa habari za kughushi ni kuamini habari nyingi. Nyingi zina kiini cha ukweli, lakini mara nyingi huhitimisha hitimisho lisilo na ukweli. Simulizi nyingi za habari za kughushi zimeundwa ili kusababisha mshtuko*. Hii inamaanisha kuwa unahitaji kuweka hisia zako wakati unasoma, ukiangalia, au unazisikiliza. Jaribu kuzipitia habari hizo katika hali ya ukosoaji na kila wakati jiulize:

  • Kwa nini hadithi hii iliandikwa?
  • Je, inajaribu kunishawishi kuwa na maoni fulani? (Kumbuka kuwa maoni ya mhariri au vipande vya maoni * ni kawaida katika magazeti, redio, na haswa mtandaoni. Kwa mfano, mwanasiasa mstaafu au mwanasayansi anayejulikana vizuri au mwandishi wanaweza kutoa maoni yao juu ya mada). Wakati mwingine, simulizi za habari huandikwa kwa njia ambayo imekusudiwa kuwashawishi wasikilizaji au msomaji wa maoni fulani na labda ya kisiasa—bila kubainisha kwamba hadithi hiyo ni maoni ya mtu mmoja tu.
  • Je, inajaribu kupata mrejesho fulani kutoka kwangu? Kwa mfano, redio au gazeti au habari ya kwenye mtandao inaweza kuorodhesha mafanikio na nguvu za mwanasiasa bila kutaja makosa yao katika juhudi (isiyojulikana) ya kushawishi hisia zako na kupata kura yako katika uchaguzi ujao.
  • Je, inajaribu kuniuzia bidhaa fulani?
  • Je, inajaribu kunifanya nibofye kwenye tovuti au kushirikisha habari mimi mwenyewe?

Ikiwa jibu lako kwa swali lolote kati ya haya ni “ndio,” angalia kwa kina zaidi habari hiyo kabla ya kuishirikisha.

Angalia chanzo

Ikiwa unaona habari kutoka kwenye chanzo ambacho hafahamiani nacho, fanya utafiti. Tafuta: Je, imechapishwa na chombo cha habari cha kitaalam au mwandishi wa habari aliyeidhinishwa? Je, inatoka kwenye blogu za kiholela?

Habari nyingi halali zinazotolewa hujumuisha nukuu na sifa kutoka kwa vyanzo vya kuaminika ili kuongeza uaminifu na ni pamoja na mitazamo mbali mbali katika habari. Ikiwa habari haina vyanzo, uwezekano ni kwamba unasoma kipande cha maoni au aina fulani ya habari ya kughushi.

Ikiwa habari imechapishwa na tovuti ya habari ambayo hauifahamu, kuwa mwangalifu. Angalia sehemu ya tovuti “Kuhusu sisi” na jaribu kuhakiki kama kampuni ina wafuasi wanaoifuatilia au imeunganishwa au kufadhiliwa na mashirika au watu binafsi wenye watu wengi wanaowafuatilia. Pia, angalia katika ukurasa wa “wasiliana nasi”. Inapaswa kuwa wazi ni nani anamiliki, anafadhili, na anadumisha tovuti. Kwa mfano, unapaswa kuhoji uhalali wa tovuti ikiwa anwani ya barua pepe ni akaunti ya gmail!

Kengele za ving’ora zinapaswa pia kulia ikiwa URL ya tovuti* inaonekana isiyo ya kawaida. Kwa ujumla, URL zilizo na majina ya kawaida ya kikoa kama .com, .org, .ac, .gov, .net au kikoa cha kiwango cha juu cha msimbo wa nchi (Kwa mfano, .gh kwa Ghana na .ml kwa Mali) ni za kuaminika, wakati URL za tovuti zilizo na majina ya kikoa yasiyojulikana au marefu haziwezi kuwa hivyo. Baadhi ya tovuti za habari za kughushi kiuhalisia zinanakili habari ambazo ni halali. Ikiwa URL, nembo, au muundo unaonekana kutokuwa kawaida, inafaa kutazama kwa ukaribu.

Pia, angalia habari zingine ambazo tovuti imechapisha. Ikiwa, kwa mfano, unagundua kwamba wingi wa habari zao umezidisha vichwa vya habari, yaliyomo ndani hayaaminiki, picha zinazotisha, au picha za watu walio uchi, unapaswa kuwa mwangalifu kuiamini na kushirikisha habari hiyo.

Angalia ni nani mwingine anayeripoti habari hiyo

Ikiwa ni habari ya kimataifa, angalia kila wakati ili kuona ikiwa imechapishwa na mashirika ya habari yenye kuheshimiwa kama vile BBC, Al Jazeera, CBC, Reuters, CNN, RFI, AllAfrica.com, nk. Ikiwa sivyo, kuna uwezekano kwamba yote au sehemu ya habari inaweza kuwa sio ya kweli. Mashirika kama haya yanaangalia na kuhakikisha kila habari kabla haijatangazwa au kuchapishwa. Ikiwa hawaitangazi habari hiyo, kuna uwezekano kwamba ni ya kughushi.

Kwa habari za ndani, angalia kwanza ikiwa habari hiyo imechukuliwa na wachapishaji wengine wanaojulikana na wenye kuheshimiwa katika nchi yako.

Angalia ushahidi

Simulizi ya habari inayoaminika daima ina ukweli mwingi, pamoja na nukuu kutoka kwa wataalam, tafiti, na takwimu rasmi. Ikiwa haya hayapatikani au chanzo ni “mtaalam” ambaye hajabainishwa au “watu katika tukio” ni shaghala baghala unapaswa kuhoji usahihi wa habari.

Uandishi wa habari wa kweli unaendeshwa kwa kukusanya ukweli, kwa hivyo ukosefu wa utafiti labda unamaanisha ukosefu wa habari zenye ukweli. Kukosekana kwa nukuu kutoka kwa watu ambao wanahusika sana na habari hiyo mara nyingi ni ishara ya “kipande cha maoni,” kilichochapishwa kama chapisho la blogu au safu, ambayo inaweza kuwa habari ya kughushi. Pia, mashirika ya habari za kuaminika yana uwazi: Ikiwa hawana ukweli wote juu ya habari, wanakiri, kwa mfano, wanaripoti kwamba wamejaribu kuwasiliana na chanzo lakini hawajapata mrejesho.

Jaribu tovuti za kuangalia ukweli wa habari kama https://africacheck.org/ na Snopes.com. Tovuti hizi zipo kwa ajili ya kupata ukweli.

Angalia ni nani aliyeiandika

Fanya uchunguzi wa haraka ili kuona ikiwa mwandishi amechapisha nakala zingine zozote. Ikiwa hawana, au nakala hiyo ina mtu mashuhuri au mwandishi hajulikani, tia shaka!

Wakati mwingine, habari zinaweza kuenea baada ya kusambazwa na mtu mashuhuri wa uwongo – kupitia akaunti ya mtandao wa kijamii iliyotengenezwa kwa ajili ya kumuiga mhusika halisi/wa kweli.

Angalia tarehe

Kwa mtazamo wa kwanza, nakala ya habari inaweza kuonekana kuwa ya kweli kwa asilimia miamoja (100%). Chanzo ni cha kuaminika, mwandishi unamfahamu, na makala hiyo imeandikwa vizuri. Hata hivyo, bado unahitaji kuwa mwangalifu… kwasababu habari hiyo inaweza kuwa imeandikwa miaka 10 iliyopita! Waundaji wa habari za kughushi mtandaoni mara nyingi huchukua habari halali lakini ya zamani na kuichapisha tena ikiwa kuna fursa ya kuimarisha au kuongeza wafuasi.

Kwa mfano, habari kuhusu ajali ya ndege kutoka mwaka 2009 inaweza kuchapishwa tena mnamo mwaka 2019 na maelezo ambayo yanaonyesha ni kitendo cha sasa cha ugaidi. Picha hiyo inaweza kusambazwa ili kuwadanganya watu kufikiria kwamba kulikuwa na kitendo cha hivi karibuni cha kigaidi nchini Merika na kutetea kuongeza matumizi ya kupambana na ugaidi au kukomesha uhuru wa raia. Vivyo hivyo, picha zinaweza kutumiwa kueneza habari zisizo za kweli. Kwa mfano, picha ya umati wa watu kutoka katika tukio la zamani inaweza kusambazwa na kuunganishwa na tukio la hivi karibuni ili kuongeza au kupunguza umaarufu uliotambuliwa wa maandamano au mkutano wa hadhara.

Angalia picha

Programu za kisasa za kopyuta za kuhariri kama vile Photoshop hufanya iwe rahisi kwa watu kuunda picha za kughushi zinazoonekana kuwa za kweli. Zingatia ishara za onyo kama vivuli vinavyoelekeza mwelekeo usiofaa, kando ya sura iliyozunguka umbo, tofauti za rangi, au sehemu ya nyuma ya picha ambayo hailingani kabisa na sehemu ya mbele ya picha.

Tovuti zingine za habari za kughushi hutumia picha za kusumbua au mchoro wa picha za makusudi kuwavuta wasomaji kusoma habari hiyo. Au, kama ilivyotajwa hapo juu, wanachukua picha zenye ushawishi kutoka kwa habari ya zamani na ya kweli, halafu wanaitumia tena kwenye habari ya kughushi.

Ikiwa una shaka, jaribu kutafuta picha hizo kupitia Google na uone ikiwa zimeunganishwa kwenye habari zingine.

Video zinaweza pia kutumika kama habari isiyo ya kweli. Hapa kuna mfano wa kina kirefu wa habari ya kughushi * inayoonyesha hili.

Angalia ubora

Ukigundua uwekaji wa alama za vituo umezidi ?!!!!!????!!??!!??! au alama za kuonyesha hisia —endelea kuwa na tahadhari. Vyanzo vya habari vinavyojulikana kawaida huhakikisha kuwa nakala zote zinaangaliwa kabla ya kuchapishwa au kutangazwa. Vile vile kwenye video —weka umakini na ishara za picha za kufundishwa.

Hakikisha kichwa cha habari kinalingana na habari yenyewe

Vichwa vyote vya habari za kughushi vinaweza kuwa kwa herufi kubwa ili kuchukua umakini wako na kusababisha majibu ya mhemko. Lakini unaposoma zaidi au kubonyeza kwenye kiungo cha habari, au ukiangalia video kwa uangalifu zaidi, wakati mwingine unaona kuwa habari hiyo haihusiani kabisa na kichwa cha habari.

Soma kila wakati kiini cha habari kwa uangalifu-usidhani tu kwamba kichwa cha habari na aya ya ufunguzi vinaendana. Vinginevyo, unaweza kuchukua habari nnje kabisa ya muktadha.

Habari za kughushi mara nyingi hubuniwa ili kuongeza mgawanyiko kati ya vikundi viwili au zaidi vya watu wenye asili tofauti au maoni tofauti, na kuchochea ubaguzi na mizozo ya kijamii. Ikiwa kichwa cha habari kinaonyesha shari na kinaonekana kimeundwa ili kuchochea hasira au woga, kuna nafasi kubwa kwamba habari hiyo sio ya kweli.

Tumia akili ya kawaida

Mwishowe, ikiwa habari inasikika sana-juu au isiyoaminika… labda ni!

Habari za kughushi mara nyingi huandaliwa ili kushawishi maoni yako, kutoa hisia kali kuelekea kitu fulani au mtu, kuongeza hofu yako na upendeleo, na kuunda mawazo yako yaendane na maoni fulani. Wakati mwingine, labda unaweza kutaka habari kuwa ya kweli, kwa sababu inathibitisha maoni yako mwenyewe au inasikika kuwa nzuri. Lakini kumbuka: kwa sababu hadithi inapatikana kwenye tovuti au inatangazwa kwenye redio au Televisheni au imetolewa katika magazeti-au hata imetolewa na rafiki anayeaminika — haimaanishi kuwa ni kweli.

Na kumbuka, kwa sababu habari inaendana vizuri na mtazamo wako mwenyewe juu ya mambo haimaanishi kuwa ni kweli. Hizi ndizo habari ambazo lazima uwe macho zaidi!

2. Usiwe sehemu ya tatizo

Daima ni wazo nzuri kuchukua muda ili kuangalia uhalisia wa habari na uangalie ukweli. Kumbuka kwamba habari za kughushi unazoeneza zinaweza kusababisha madhara makubwa kwa watu binafsi, kwa mazingira halisi. Inaweza pia kuathiri uaminifu wako na uaminifu wa kituo cha redio unachofanyia kazi. Hautakiwi kueneza uvumi na kuwajibika kwa kufanya watu waamini jambo ambalo si kweli.

Linapokuja suala la kuripoti habari, daima kuwa sahihi na mwenye maadili. (Angalia viwango vya USAWA vya Farm Radio hapa.) Jaribu kuambatana na miongozo ifuatayo:

  • Tafuta ukweli na uripoti kwa haki na usahihi.
  • Kuwajibika na kuwa muwazi, kwa mfano, kukubali na kuomba msamaha pale unapokosea, kuchapisha habari za ufuatiliaji ambazo hushughulikia ripoti mbaya na kusema wazi umiliki na mrengo wa kisiasa wa kituo hicho, nakala au mmiliki. Tazama hapa kuona namna ya kuomba msamaha kutoka gazeti la New York Times, na hapa kutoka katika gazeti la Daily Nation (Uganda).
  • Punguza adhari na uwatendee watu wote kwa heshima sawa.
  • Usipotoshe au kuzidisha ukweli au muktadha.
  • Daima linganisha vyanzo vingi na usitegemee vyanzo visivyojulikana.

Ongea!

Watoa habari na wapokea habari wana jukumu la kushughulikia habari za kughushi. Ikiwa unaona habari ya kughushi au maudhui yenye kutilia shaka, chukua hatua zozote zinazowezekana kwa upande wako. Hii inaweza kumaanisha kutoirusha hewani au vinginevyo kutoeneza habari hiyo. Wakati mwingine, unaweza hata kumfikia mtu aliyeshiriki habari hiyo na kuanza mazungumzo juu ya kwanini unafikiri yaliyomo kwenye habari hiyo hayaonekani kuwa ya kuaminika. Aina hizi za jitihada zinaweza kusaidia wengine kuepuka kuanguka katika mtego wa habari za kughushi.

3. Umuhimu wa ukweli

Katika umri mdogo, tunafundishwa kuwa kusema ukweli ni muhimu. Ukweli ni dhana muhimu kwa watangazaji na waandishi wa habari. Ukweli ni kwamba vyama vya waandishi wa habari vimeanzisha miongozo ya maadili ambayo waandishi wa habari wanaweza kufuata ili kuambatana na ukweli. Miongozo hii itakuwezesha kupata uaminifu na heshima kutoka kwa wasikilizaji wako.

Wakati kila mtu anapaswa kuwa na haki na maoni yake na huru kuchangia mjadala wa umma, ni muhimu sana kwa waandishi wa habari na watangazaji kuwa na ujuzi wa kutofautisha kati ya habari za kughushi na habari ambayo ni taarifa halali. Ni muhimu pia kwamba waandishi wa habari na watangazaji wafanye maamuzi sahihi kuhusu ni muda kiasi gani wa hewani wanatoa kwa maoni tofauti na vikundi tofauti. Kwa mfano, wakati ni kweli kwamba kila mtu ana haki na maoni yake, kuhusu maswala ya kisayansi kama mabadiliko ya tabia ya nchi, maoni ya wanasayansi halali wa hali ya hewa yana uzito zaidi kuliko yale ya wasio wanasayansi, na matangazo yako yanapaswa kuakisi hilo. Hii ni muhimu kwa sababu waandishi wa habari na watangazaji wanaweza kuchangia kueneza hoja za uwongo na maoni ambayo yanaweza kuathiri afya ya binadamu na mazingira ya asili.

Umma unategemea watangazaji kama wewe kwa habari sahihi juu ya kile kinachoendelea katika kijiji chako, mji, jiji, au mkoa. Kwa hivyo ni jukumu lako kuchukua muda kukusanya ukweli kabla ya kuripoti juu ya habari. La sivyo, wasikilizaji wako wanaweza kugeukia chanzo kisichoaminika zaidi na chenye ufahamu mdogo wa eneo hilo, na hiyo inaweza kusababisha wao kupotoshwa.

Kupoteza imani kwenye chombo cha habari kunaweza kudhoofisha mjadala wa umma wenye nafasi ya kuchochea hatua stahiki kwa maslahi ya umma. Kujua jinsi ya kuona habari za kughushi na nini cha kufanya juu yake kunahitaji kuwa muangalifu, lakini inastahili. Kama mtangazaji, uaminifu na usahihi ni zana za biashara yako.

 

Wapi pengine naweza kujifunza kuhusu habari za kughushi?

 

  1. Arc du Canada (Alliance des radios communitaires), 2018. Fausses nouvelles : 5 questions à vous poser pour éviter d’en partager. https://radiorfa.com/index.php/fausses-nouvelles-5-questions-pour-eviter-partager/
  2. BBC Newsround, undated. Fake News: What is it? And how to spot it. https://www.bbc.co.uk/newsround/38906931
  3. Bellemare, Andrea, 2019. The real ‘fake news’: how to spot misinformation and disinformation online. Canadian Broadcasting Corporation. https://www.cbc.ca/news/technology/fake-news-misinformation-online-1.5196865
  4. Bellemare, Andrea, 2019. So, you think you’ve spotted some ‘fake news’ — now what? Canadian Broadcasting Corporation. https://www.cbc.ca/news/technology/fake-news-disinformation-propaganda-internet-1.5196964
  5. Berdik, Chris, 2016. How to Teach High-School Students to Spot Fake News. https://slate.com/technology/2016/12/media-literacy-courses-help-high-school-students-spot-fake-news.html
  6. British Council, undated. How to Spot Fake News. https://learnenglish.britishcouncil.org/intermediate-b1-reading/how-to-spot-fake-news
  7. Charlton, Emma, World Economic Forum, 2019. Fake News: What it is, and how to spot it. https://www.weforum.org/agenda/2019/03/fake-news-what-it-is-and-how-to-spot-it/
  8. EAVI, undated. Infographic: Beyond Fake News – 10 Types of Misleading News – Sixteen Languages. https://eavi.eu/beyond-fake-news-10-types-misleading-info/
  9. Mackintosh, E., 2019. Finland is winning the war on fake news. What it’s learned may be crucial to Western democracy. CNN (Cable News Network). https://edition.cnn.com/interactive/2019/05/europe/finland-fake-news-intl/
  10. McGonagle, Tarlach, NQHR, 2017. Fake News: False Fears or Real Concerns? https://journals.sagepub.com/doi/pdf/10.1177/0924051917738685
  11. McManus, Melanie Radzicki, How Stuff Works, undated. 10 Ways to Spot a Fake News Story. https://history.howstuffworks.com/history-vs-myth/10-ways-to-spot-fake-news-story.htm
  12. Mind Tools, undated. How to Spot Real and Fake News. https://www.mindtools.com/pages/article/fake-news.htm
  13. Nagler, Christina, Harvard University, undated. 4 Tips for Spotting a Fake News Story. https://www.summer.harvard.edu/inside-summer/4-tips-spotting-fake-news-story
  14. National Observer, undated. How to spot fake news. https://www.nationalobserver.com/spot-fake-news
  15. Posetti, J. and Matthews, A., 2020. #CoveringCOVID: Six Recommendations for Disinformation Combat. ICFJ (International Center for Journalists). https://www.icfj.org/news/coveringcovid-six-recommendations-disinformation-combat
  16. Selini, Alberto, 2019. Pour répondre à la désinformation, il faut d’abord se poser les bonnes questions. EJO (European Journalism Observatory). https://fr.ejo.ch/deontologie-qualite/pour-repondre-desinformation-se-poser-les-bonnes-questions-fake-news-ethique-disinformation
  17. Society of Professional Journalists, 2014. SPJ Code of Ethics. https://www.spj.org/ethicscode.asp
  18. Waugh, Rob, The Telegraph, 2019. 10 Tips on How to Spot Fake News. https://www.telegraph.co.uk/technology/information-age/how-to-spot-fake-news/
  19. White, Aidan, undated. Fake News: Facebook and Matters of Fact in the Post-Truth Era. https://ethicaljournalismnetwork.org/resources/publications/ethics-in-the-news/fake-news

Sauti

Africa angalia. Sauti na matangazo (kutoka vituo vya redio vya Africa na hasa juu ya COVID-19). https://africacheck.org/spot-check/audio-and-podcasts/

 

Ufafanuzi

 

Mwanablogu: Mtu anayeandika blogu mtandaoni (rekodi ya kawaida ya maoni, mawazo, au uzoefu ambao umechapishwa kwenye tovuti ili watu wengine wasome).

Boti: Ni kifupisho cha neno Roboti; Ni programu ya kujitegemea kwenye mtandao (haswa intaneti) ambayo inaweza kuingiliana na mifumo ya kompyuta au watumiaji.

Chambo (Clickbait): (kwenye Intanet), maudhui ambayo kusudi lake kuu ni kuvutia umati na kuhimiza wanaotembelea mtandao kubonyeza kwenye kiunga cha ukurasa fulani wa tovuti.

Habari ghushi za kina: Habari ghushi (kutoka “Kujifunza kwa kina” na “ghushi”) ni vyombo vya habari vya kughushi ambavyo mtu katika picha au video iliyopo hubadilishwa na sura ya mtu mwingine.

Habari zisizo za kweli: Habari ya uwongo wa makusudi na mara nyingi huenea kwa kuficho (kwa mfano, uenezaji wa uvumi) ili kushawishi maoni ya umma au kuficha ukweli.

GIF: Ni kifupisho cha neno la kingereza “Graphic Interchange Format”; picha ambazo zimesimbwa kwa kutumia muundo wa kubadilishana picha ambapo zina fremu nyingi zilizoingizwa kwenye faili moja ya picha na kivinjari cha tovuti au programu nyingine itacheza picha hizo nyuma moja kwa moja katika mlolongo wa michoro.

Mlipuko wa habari (Going viral): Wakati ambapo nakala, video, au picha inaenea haraka na kwa urahisi kwenye tovuti kupitia mitandao ya kijamii au barua pepe.

Habaripicha: Picha ya kuona kama chati au mchoro unaotumika kuwakilisha habari au data.

Meme: Sehemu ya kitamaduni au mfumo wa tabia ambao unaweza kuchukuliwa kama umepitishwa kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine kwa njia zisizo za kimaumbile, haswa kuiga.

Kipande cha maoni: Nakala ambayo waandishi wanaelezea maoni yao binafsi juu ya suala fulani au habari, kwa kawaida ni habari ambayo ni ya ubishani au ya kuchochea.

Photoshop: Programu ya kuhariri ambayo inawezesha ubadilishaji wa picha za dijiti. Imetolewa na Shirika la Adobe.

Habari ya Mshtuko (Shock value): Wakati picha, maandishi, makala, au video inasababisha kero kama chukizo kali, mshtuko, hasira, woga, au hisia kama hizo.

URL: Ni kifupisho cha neno la kingereza “Uniform Resource Locator” – inayojulikana zaidi kama anwani ya tovuti ambayo inabainisha eneo lake kwenye mtandao wa kompyuta.

Uandishi wa habari wa Manjano (Yellow journalism): Uandishi wa habari ambao umejikita katika uhasama na uzushi mbaya. Kwa mfano, kulinganisha mauaji na tukio la mtu kukatwa kiungo kutokana na uvutaji wa bangi ni aina mbaya zaidi ya uandishi wa habari wa manjano.

Acknowledgements

Shukrani

Imechangiwa na: Andy Everett, Mhariri Msaidizi, Heart FM, UK, Sylvie Harrison, Meneja, Radio Craft, Farm Radio International, na Vijay Cuddeford, Mhariri msimamizi, Farm Radio International

This resource is undertaken with the financial support of the Government of Canada provided through Global Affairs Canada.